Na Apostle Darmacy
Takwimu zilizotolewa katika kikao cha Baraza la Waangalizi wa Kanisa la
Tanzania Assemblies of God (TAG), kilichofanyika mjini Dodoma siku
kadhaaa zimepita, zinaonesha kukua kusiko kwa kawaida katika kipindi cha
miaka mitano iliyopita, na kuwashangaza hata watu kutoka mataifa
yaliyotangulia kupata muamko wa Injili kama vile Marekani.
Takwimu hizo zinaonesha ongezeko la kila eneo kwa zaidi ya asilimia 100,
katika kipindi cha miaka mitano tu yaani kuanzia mwaka 2008-2013,
mfano; mwaka 2008, kanisa lilikuwa na Sehemu (section) 75, na sasa lina
Sehemu 226.
Hadi kufika mwishoni mwa mwaka jana, kanisa hilo linaloongozwa na dira
yake ya maendeleo ya ‘Miaka 10 ya Mavuno’ lilikuwa na watumishi wenye
vyeti mbali mbali 5,026, na makanisa 5007, yaliyoenea nchi nzima na
kulifanya kuwa kanisa kubwa na linalokua kwa kasi zaidi miongoni mwa
yale ya Kipentekoste Tanzania.
Jambo lililolipua shangwe za wajumbe wa baraza hilo kutoka kila kona ya
Tanzania, ni ukweli kuwa ukuaji wa kanisa unakwenda sambamba na ukuaji
wa elimu, ujenzi na upanuzi wa Vyuo vya Biblia, vya kupanda makanisa na
msisitizo wa kimaadili.
 |
| Askofu Mkuu wa TAG, Dk. Barnabs Mtokambali |
Takwimu pia zinaonesha kuwa, kanisa hilo limekuwa kiidadi likiongezeka
kwa zaidi ya asilimia 200, tangu lilipozindua dira yake ya maendeleo
iliyoweka lengo la kufikia kila roho inayopotea dhambini Tanzania.
Akisoma taarifa hiyo, mbele ya mamia ya wajumbe wa bbaraza hilo, Katibu
Mkuu wa TAG, Rev. Ron Swai, alisema kuwa, hadi kufika Desemba mwaka
jana, watenda kazi 2280, walikuwa tayari wamehitimu masomo katika vyuo
vya kupanda makanisa na kuingia shambani kumtumikia Mungu.
Katika kipindi hicho, kanisa limeweza kununua magari ya thamani kwa
maaskofu wake nchi nzima, wakurugenzi wa Idara, na sasa mradi wa kugawa
piki piki kwa waangalizi, tayari umeanza ambapo baadhi yao walitarajiwa
kukabiziwa vyombo hivyo vya kurahisisha utumishi katika kazi ya Bwana
Ijumaa iliyopita mjini Dodoma.
Pamoja na vyombo vya usafiri, kanisa hilo limejikita katika Uinjilisti,
likiwanunulia Wainjilisti wa kitaifa vyombo vya kisasa vya kuhubiria
pamoja na vifaa maalumu vya uinjilisti kwa njia ya sinema ili kuwafikia
watanzania wote. Mradi huo wa ununuzi wa piki piki za kisasa aina ya
Yamaha, kutoka Japani utagharimu shilingi milioni 800,na tayari Askofu
Mkuu wa TAG, Dk. Barnabs Mtokambali amepata mshirika katika kazi ya
Mungu atakaye gharamia mradi huo.
Ni kwa kuguswa na matokeo chanya ya dira ya maendeleo ya Kanisa la TAG,
Mtumishi wa Mungu kutoka Marekani, Dk. David M. Oliver, ambaye pia ni
rais wa huduma ya Living Water LLC, yenye makao yake North Canton Ohio
Marekani, aliwaambia mamia ya waangalizi hao kuwa wanapaswa kumshukuru
sana Mungu kwa kuwapa viongozi wa kanisa wenye wingi wa hekima na maono
makubwa ya kulifikisha mbali kanisa.
Dk. Oliver alikuwa akifundisha somo linalohusu Nguvu ya Uponyaji wa
Baraka-Mwongozo wa kusikiliza, ambapo alianza kwa kufafanua maana ya
Neno Baraka.
“Neno Baraka linatokana na neno la kilatini ‘benedicere’ likiwa na
maana ya kusema kitu vizuri, ‘kusifu’ ‘inua’ au kutakia mema,”alifafanua
Dk. Olvier katika somo lake hilo.
Huku akinukuu Maandiko Matakatifu kutoka vitabu vya Warumi 5:8 na Yohana
11:25-26, alisisitiza: “Lazima tujifunze kuishi kwa neema, rehema na
Baraka za Mungu, bila kujaribu kupata utajiri kutokana na hivyo. Baraka
msingi wake ni kweli na hubeba nguvu ya Mungu…..”
Dk. Oliver alifundisha kwa kina misingi ya baraka za Mungu na jinsi ya
kupokea na kubariki wengine, akitoa mifano kadhaa ya maisha na utumishi
wake.
Toa Maoni Hapa Chini