


Ni Moja ya Mafundisho/ masomo kwa Vijana.
“Mara nyingi ngono
ya kinywa huongoza kwenye ngono, na vijana wengi huiona kuwa salama
kuliko ngono ya kawaida . . . na njia ya kuepuka kupata mimba na
kudumisha ubikira wao.” Pia
vijana wengine huepuka ngono
lakini wanajihusisha katika matendo mengine yanayohusiana na ngono kama
vile kupapasana viungo vya uzazi.
(Waebrania 13:4)
Uchunguzi mmoja uliofanywa katika nchi moja ya Asia ulifunua kwamba
wavulana wengi kati ya umri wa miaka 15 na 24 wanahisi kwamba kufanya
ngono kabla ya ndoa si jambo linalokubalika tu bali pia linatazamiwa. Haishangazi kwamba vijana wengi ulimwenguni pote hufanya ngono kabla ya kufikia umri wa miaka 19.
Mkristo anapaswa kuonaje ngono
kabla ya ndoa? Na vipi matendo mengine yanayohusiana na ngono? Je, Mungu
anayakubali? Je, ni salama? Na je, kweli yanadumisha ubikira?
Maana ya Uasherati

Muumba wetu, Yehova Mungu, ndiye
anayeweza kuweka viwango kuhusiana na mambo hayo. Katika Neno lake
anatuambia ‘tuukimbie uasherati.’ (1 Wakorintho 6:18)
Hilo linamaanisha nini? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “uasherati”
halihusu tu ngono bali linatia ndani matendo mengine machafu
yanayohusiana na ngono. Kwa hiyo, ikiwa watu wawili wasiooana
wanajihusisha katika ngono ya kinywa au kupapasana viungo vya uzazi, wanafanya uasherati.
Je, bado Mungu atawaona kuwa mabikira? Neno “bikira”


hutumiwa katika Biblia kuonyesha usafi wa maadili. (2 Wakorintho 11:2-6)
Lakini linatumiwa kihalisi pia. Biblia inazungumzia msichana mmoja
aliyeitwa Rebeka. Inasema kwamba alikuwa “bikira, wala hakuna mwanamume
aliyekuwa amelala naye.” (Mwanzo 24:16)
Katika Kiebrania cha awali, neno “ngono” lilihusisha matendo mengine
zaidi ya ngono ya kawaida kati ya mwanamume na mwanamke. (Mwanzo 19:5) Kwa hiyo, kulingana na Biblia, kijana akijihusisha katika aina yoyote ya uasherati, hataonwa kuwa bikira.
Zaidi ya kuwahimiza Wakristo wajiepushe na uasherati, Biblia huwahimiza wajiepushe na matendo machafu ya aina zote ambayo yanaweza kuongoza kwenye uasherati.* (Wakolosai 3:5)
Huenda ukadhihakiwa kwa kuchukua msimamo huo. Kijana mmoja Mkristo
anayeitwa Kelly anasema: “Nilipokuwa katika shule ya sekondari, sikuzote
niliambiwa, ‘Hujui kile unachokosa!’” Hata hivyo, ngono kabla ya ndoa
ni “kufurahia dhambi kwa muda.” (Waebrania 11:25) Inaweza kusababisha madhara ya kudumu ya kimwili, kihisia, na kiroho.
Madhara Makubwa
Biblia inatueleza kwamba wakati
mmoja Mfalme Sulemani alimwona kijana akishawishiwa kufanya ngono kabla
ya ndoa. Sulemani alimlinganisha kijana huyo na “ng’ombe-dume anayeenda
machinjoni.” Ng’ombe-dume anayeenda kuchinjwa hajui kitakachompata. Mara
nyingi vijana wanaojihusisha na ngono kabla ya ndoa hutenda vivyo
hivyo, kana kwamba hawajui madhara makubwa yatakayowapata! Sulemani alisema hivi kuhusu kijana huyo: “Hajajua kwamba nafsi yake mwenyewe inahusika.” (Methali 7:22, 23) Naam, “nafsi” yako, yaani, uhai wako umo hatarini.
Kwa mfano, kila mwaka mamilioni
ya vijana hupata magonjwa ya zinaa. Lydia anasema: “Nilipojua kwamba
nina ugonjwa fulani wa zinaa ambao husababisha vidonda,
nilitaka kutoroka.” Anajuta hivi: “Ni ugonjwa unaosababisha maumivu
makali sana na hauwezi kuponywa.” Zaidi ya nusu ya watu wanaoambukizwa
virusi vya UKIMWI ulimwenguni pote (6,000 kwa siku) wana umri wa kati ya
miaka 15 na 24.
Wanawake hasa ndio wanaokumbwa
zaidi na matatizo yanayosababishwa na ngono kabla ya ndoa. Kwa kweli,
wanawake ndio wanaokabili uwezekano mkubwa wa kupata magonjwa ya zinaa
(kutia ndani virusi vya UKIMWI) kuliko wanaume. Msichana mdogo akipata
mimba, yeye pamoja na mtoto wake aliye tumboni wamo hatarini. Kwa nini?
Kwa kuwa mwili wa msichana huyo haujakomaa vya kutosha kuweza kujifungua
bila matatizo yoyote.
Hata msichana huyo akiepuka matatizo makubwa ya afya, bado atakabili madaraka makubwa ya kuwa mzazi. Wasichana wengi huona kwamba kujiruzuku na kumtunza mtoto ni kazi ngumu sana kuliko walivyofikiri.
Kisha kuna madhara ya kiroho na
kihisia. Dhambi ya uzinzi ya Mfalme Daudi ilihatarisha uhusiano wake
pamoja na Mungu na alikuwa karibu kuangamia kiroho. (Zaburi 51) Ingawa Daudi alipona kiroho, alipata madhara ya dhambi yake muda wote wa maisha yake.
Vijana wanaweza kupatwa na
madhara yayo hayo leo. Kwa mfano, Cherie alifanya ngono na mvulana
fulani alipokuwa na umri wa miaka 17. Alifikiri kwamba mvulana huyo
alimpenda. Miaka kadhaa imepita lakini bado anajutia matendo yake.
Anasema hivi kwa masikitiko: “Nilipuuza kweli za Biblia na kupata
madhara. Nilipoteza kibali cha Yehova, na hilo liliniumiza sana.” Kijana
anayeitwa Trish anakubali hivi pia: “Kosa kubwa nililofanya maishani ni
kufanya ngono kabla ya ndoa. Ninatamani sana kuwa bikira tena.” Naam,
madhara ya kihisia yanaweza kudumu kwa miaka mingi na kusababisha
mfadhaiko na huzuni.
Kujifunza Kujizuia
Msichana anayeitwa Shanda
anazusha swali hili muhimu, “Kwa nini Mungu awape vijana tamaa ya ngono,
akijua kwamba hawapaswi kuitosheleza kabla ya ndoa?” Ni kweli kwamba
tamaa ya ngono inaweza kuwa yenye nguvu sana wakati wa “upeo wa ujana.” (1 Wakorintho 7:36)
Kwa hakika, vijana wanaweza kupata tamaa ya ngono ghafula bila sababu
yoyote. Lakini hiyo si dhambi. Hilo ni jambo la kawaida katika ukuzi wa
viungo vya uzazi.*
Pia ni kweli kwamba Yehova
alikusudia mahusiano ya ngono yafurahishe. Hilo linapatana na kusudi
lake la awali kwamba wanadamu waijaze dunia. (Mwanzo 1:28)
Hata hivyo, Mungu hakukusudia tutumie vibaya nguvu zetu za uzazi.
Biblia inasema: “Kila mmoja wenu ajue jinsi ya kukiweza chombo chake
mwenyewe katika utakaso na heshima.” (1 Wathesalonike 4:4) Ni upumbavu kutosheleza kila tamaa ya ngono kwani ni kama kumpiga mtu kila unapokasirika.
Mahusiano ya ngono ni zawadi
kutoka kwa Mungu ambayo inapaswa kufurahiwa wakati unaofaa, yaani, baada
ya mtu kufunga ndoa. Mungu anahisije tunapojaribu kufurahia ngono kabla
ya ndoa? Wazia umemnunulia rafiki yako zawadi, lakini kabla ya kumpa
anaiiba! Je, hungekasirika? Fikiria jinsi Mungu anavyohisi mtu
anapofanya ngono kabla ya ndoa na kutumia vibaya zawadi ambayo Mungu
ametoa.
Ufanyeje kuhusu hisia zako za
ngono? Jifunze kuzizuia. Kumbuka kwamba “Yehova mwenyewe hatawanyima
jambo lolote jema wale wanaotembea bila kosa.” (Zaburi 84:11)
Kijana anayeitwa Gordon anasema: “Ninapoanza kufikiri kwamba si vibaya
kufanya ngono kabla ya ndoa, mimi hutafakari kuhusu madhara ya kiroho
na kutambua kwamba sipaswi kuruhusu dhambi yoyote iharibu uhusiano
wangu na Yehova.” Huenda isiwe rahisi kujizuia. Lakini kama vile kijana
anayeitwa Adrian anavyotukumbusha, “kujizuia hukuwezesha kuwa na dhamiri
safi na uhusiano mzuri na Yehova, na kukazia fikira mambo ya maana
zaidi bila majuto wala masikitiko yoyote.”—Zaburi 16:11.
Kuna sababu nyingi nzuri za ‘kujiepusha na uasherati’ wa aina yoyote. (1 Wathesalonike 4:3)
Ni kweli kwamba si rahisi kufanya hivyo nyakati zote. Makala ya wakati
ujao itazungumzia jinsi unavyoweza ‘kujihifadhi ukiwa safi kiadili.’—1 Timotheo 5:22.
Kwa Maoni na ushauri wasiliana na Apostle Darmacy
e-mail damasdogan@gmail.com
Toa Maoni Hapa Chini