Wamefariki Ni Katika Ajali ya Feri
Ni katika Mto Nile wakati wakikimbia mapigano katika mji wa
Malakal.
Wananchi wa Sudan kusini wakikimbia mapigano
Taarifa zinazopatikana kutoka Sudan Kusini zinasema watu kati ya 200 na
300, ikiwa ni pamoja na wanawake na watoto wamekufa maji katika ajali
hiyo ya feri. Chombo hicho kilikuwa na watu wengi kuliko uwezo wake,
amesema msemaji wa jeshi Philip Aguer.
Ameongeza kuwa wote wamefariki. Walikuwa wakikimbia mapigano ambayo yalizuka tena katika mji wa Malakal.
Mapigano yanaendelea
Mapigano yameendelea katika maeneo mbali mbali leo(14.01.2014) katika
Sudan ya kusini . Mapigano makali yameripotiwa kutokea katika mji wa
Malakal, mji mkuu wa jimbo linalotoa mafuta kwa wingi la Upper Nile,
wakati waasi walipofanya mashambulizi mapya kuukamata mji huo, ambao
umekuwa ukibadilisha udhibiti mara mbili kati ya waasi na jeshi la
serikali tangu mzozo huo kuanza Desemba 15 mwaka jana nchini Sudan
Kusini.
Wanajeshi wa serikali wakipambana na waasi
Kuna mapigano mapya ndani na nje ya mji wa Malakal, amesema mkuu wa
misaada ya Umoja wa Mataifa kwa ajili ya Sudan kusini Toby Lanzer, na
kuongeza kuwa kituo cha jeshi la kulinda amani limefurika karibu mara
mbili ya idadi ya watu wanaohitaji hifadhi, kutoka 10,000 hadi 19,000.
Jeshi limeripoti kutokea mapigano makali kusini mwa mji wa Bor, wakati
serikali ilitaka kuudhibiti tena mji wa huo kutoka kwa waasi, mji mkubwa
pekee ambao bado uko katika udhibiti wa waasi.
Hata hivyo amekataa madai ya waasi kuwa wamekamata tena bandari ya
Mongola katika mto Nile, mji iliyopo kati ya mji wa Bor na mji mkuu
Juba.
Pia amethibitisha kuwa kumekuwa na mapigano makali kusini mwa mji mkuu, katika mji wa Rajaf jana.
Mji wa Malakal
Miili yatapakaa barabarani
Wakati huo huo miili kadha ya watu , ikiwa ni pamoja na miili ambayo
imeharibika imetapakaa barabarani kutoka uwanja wa ndege hadi katika mji
mkuu wa jimbo linalotoa mafuta kwa wingi nchini Sudan kusini la Unity.
Nyumba na majengo mbali mbali pamoja na maduka yamechomwa moto ama
kuharibiwa na kumekuwa na uporaji mkubwa, huku magari yaliyoharibiwa na
kuchomwa moto yakifuka moshi.
Matokeo ya vita mjini Bentiu na uharibifu uliotokea katika taifa hilo
jipya duniani yanaonekana wazi, wakati jeshi la serikali likiendelea
kupambana na wanajeshi ambao walilitumikia jeshi hilo mwezi mmoja
uliopita, ambao hivi sasa wanaitwa waasi.
Hayo yakiendelea viongozi wa Japan na Ethiopia wamezitaka pande
zinazopigana nchini Sudan Kusini kutia saini makubaliano ya kusitisha
mapigano ambayo yamesababisha maelfu ya watu kuuwawa.
"Tumekubaliana kuwa usitishaji wa uhasama nchini Sudan Kusini na
mapatano ya kitaifa ni muhimu sana," waziri mkuu wa Ethiopia,
Hailemariam Desalegn, amesema katika mkutano wa pamoja na waandishi
habari akiwa na mwenzake wa Japan, Shinzo Abe.
Waziri mkuu wa Ethiopia Hailemariam Desalegn
Matamshi hayo yamekuja huku mazungumzo ya amani mjini Addis Ababa kati
ya pande hasimu nchini Sudan kusini yakiendelea mjini Addis Ababa.
Ethiopia na Japan zimesema zinataka uthabiti nchini Sudan Kusini, nchi
ambayo imepata uhuru mwaka 2011 kutoka Sudan
Toa Maoni Hapa Chini