KWA TAARIFA YAKO : MTOTO WA ASKOFU KULOLA ALIVYOPITIA MAGUMU KURITHI MIKOBA YA BABA YAKE
Na Apostle Darmacy
Kati ya watoto wa Askofu Mkuu Moses Kulola, hakuna aliyekuja kudhani
kuwa Daniel Kulola, ndiye atakuwa mrithi wa kazi ya baba yao. Hata yeye
mwenyewe hakuwa anadhani hiyvo, lakini kwa taarifa yako hadi anafikia
hapo alipo, kuna mengi amepitia, magumu zaidi ya unavyoweza kudhani, na
machache kati yake ni kama ifuatavyo.
KWA TAARIFA YAKO Mchungaji Dkt Daniel Kulola hakuwa anataka kuwa
mchungaji katu, ni jambo ambalo hakulidhania - na alikuwa akichukia mno
kuwa katika huduma hiyo, lakini ilikuwa ni mwaka 1990 mwanzoni, ambapo
baba yake, yaani Askofu Moses Kulola, aliitisha kikao cha familia nzima,
na hapo ndipo mambo yalipobadilika.
Katika kikao hicho ambacho hakuna aliyejua kitakachojadiliwa, kilikuwa
kizito sana kwani baba yao alilia sana siku hiyo, akisema kuwa Mungu
amemuambia kuwa mtoto mmojawapo ndiye atakayemrithi, lakini bado hakujua
ni nani kati ya watoto wake wote. Ndipo KWA TAARIFA YAKO, mtu
mmoja akawa amechomwa sana na hayo maneno na kusimama mwenyewe na
kueleka alipo baba yake na kupiga magoti kwa ajili ya kuombewa, huo ndio
ukawa mwanzo wa huduma ndani yake, maombi yalikuwa marefu kiasi kwamba
kwa takribani wiki mbili, mkono aliowekewa Daniel ni kama bado ulikuwa
upo kichwani mwake, kwa namna ambavyo maombi yalikuwa na uzito wa
kipekee.
Kuitwa kwa Daniel hakukuwa shughuli nyepesi, kwani wachache walimuelewa huku wengi wakimshangaa na KWA TAARIFA YAKO
ni kutokana na alipokata shauri ya kuacha kazi na kugawa baadhi ya mali
zake, huku nyingine akiuza, kwa kile alichoamini kuwa vingempotezea
muda katika huduma ambayo ameitiwa.
kwa takribani miaka 8 Mchungaji Dkt Daniel Kulola alikuwa akijenga
msingi kwenye huduma, na kipindi hiki ndicho kilikuwa kipindi kigumu
mno, kwani kuna kipindi walikuwa wakilala njaa, ama pale ambapo
walishangilia kupata chakula (dona na maharage), mgeni wao akakataa kula
na kuondoka. Si hayo tu, lakini pia kuuza suti zake ili aweze kupata
nauli ya kuendea kuhubiri, licha ya kwamba sehemu nyingine aliwahi
kuacha suti zake ili ziuzwe, lakini aliporudi baada ya siku kadhaa
akakuta nguo hizo (mtaji) zimetelekezwa chini huku jua na mvua
zikiiangukia bila mtu yeyote kushtuka.
KWA TAARIFA YAKO, haya yote hayakumkwamisha wala kumzuia
kuendelea kuhubiri kutokana na kukumbuka maneno ya baba yake mzazi,
ambaye pia ni baba yake wa kiroho ya kwamba "hujaitwa na mtu, umeitwa
mwenyewe."
Waswahili husema nyani mkongwe kakwepa mishale mingi, na hakika ndivyo
ambavyo tunaweza kulinaganisha kwa mtumishi huyu wa Mungu kwani hadi
kufikia 2013, ni mambo mengi amepitia, ikiwemo ya kuvamiwa na mapepo
wakitaka kumuua akiwa madhabahuni jijini Arusha, wakati mmoja dada mmoja
aliyekuwa na pepo akamrukia mgongoni na kumng'ang'ania, huku wakati
mwingine dada mwingine aliyekuwa na mapepo akirudi kulipa kisasi baada
ya kuombewa mchana, yeye akirudi usiku na kisu mkononi ili kumuua
mchungaji Daniel. Lakini yote haya yanapita, maana hakujiita mwenyewe,
bali aliitwa kufanya kazi hii ya Mungu.
Pamoja na huduma anayofanya, Mchungaji Daniel ni msomi, na ni daktari wa thiolojia, jambo ambalo KWA TAARIFA YAKO
analihubiri sana kwa watoto wake, kwani kati ya watoto wote alionao (wa
kibaiolojia na wa kuasili), wote wanajua kuwa ugomvi na baba yao ni
pale ambapo hawasomi
Toa Maoni Hapa Chini