Askofu Dk. Kulola ataja makanisa ya shetani nchini
Na apoatle Darmacy
- Awatahadhirisha mabinti kuwa makini
- Aahidi kuwaombea akienda Israel
Askofu Mkuu wa Kanisa la Evangelistical Assemblies of God Tanzania
(EAGT) Mwinjilisti Dk. Moses Kulola, amelionya kanisa safi la Kiristo
kujitenga na wimbi kubwa la waabudu shetani wanaopenya kwa kasi
makanisani wakitumia fedha nyingi kuteka na kumiliki baadhi ya makanisa.
Kiongozi huyo pia amewataka mabinti kutulia mbele za Bwana na kufanya
ubinti wao kuwa wa utukufu wa Mungu ili siku ya mwisho Bwana ajivunie
matendo yao mema waliyoyafanya ndani ya changamoto lukuki, kwa kuwa
wanawindwa na waabudu shetani hao.
 |
| Askofu Mkuu wa (EAGT) Mwinjilisti Dk. Moses Kulola |
Askofu Kulola alisema hayo wiki iliyopita katika mahojiano maalum na
chanzo cha blog hii kilipomtembelea Chanika, nje kidogo ya jiji la Dar
es Salaam, alikokwenda kupumzika akisubiri safari ya kwenda Israel wiki
ijayo.
Askofu Kulola alisema kuwa, kanisa limevamiwa na waabudu shetani ambao
wengine wamejivika majina makubwa huku wakiendesha ibada zao wenyewe na
baba yao ibilisi, badala ya kufuata Bwana Yesu.
Huku akitaja majina ya makanisa makubwa yenye idadi kubwa ya waumini,
lakini yakiendeshwa na makundi ya siri kama Freemasons alisema umefika
wakati wa waumini kuwa makini na kusoma Biblia kwa makini huku
wakimuomba Roho Mtakatifu awanusuru.
“Wanangu natoa wito kutoka katika ibada za mashetani, ondokeni huku
wala msitazame nyuma, karibu Yesu yuaja atakuta mkimtumikia shetani kwa
kukosa maarifa ya kuzipambanua roho zidanganyazo,”alisema Askofu Kulola
na kutaja makanisa hayo ambayo majina yake ninayahifadhi kwa sasa.
Alisema kuwa kuna dini zimeibuka kama uyoga na viongozi wake
wakajipatia majina makubwa, huku wakiwa wanapewa kila kitu kutoka katika
makundi ya siri na wala sio Wakristo wa kweli.
Aliitaja miji iliyoboba katika ibada za mashetani kuwa ni Dar es
Salaam, Mwanza, Mbeya na Shinyanga, na akawahimiza Wakristo safi
waliookoka kuepuka kumeza kila fundisho kwa kuwa, hiki ni kipindi cha
kutimia kwa unabii wa Bwana Yesu kuwa siku za mwisho kutakuwepo na
makristo wa Uongo watakaofanya ishara na miujiza kiasi cha kudanganya
hata wateule.
“Ukiona kanisa linajenga fundisho lake katika miujiza pekee, badala ya
Neno na kuwaongoza watu kwenye toba na kuishi maisha matakatifu, kimbia
hilo sio la Mungu. Muujiza wa kwanza unaopaswa kutiliwa mkazo kwa nguvu
kubwa ni wenye dhambi kumpokea Yesu na kuwa wafuasi wake. Mimi sipingi
miujiza laa hasha! Lakini sio agizo kuu. Agizo kuu ni kuupa ulimwengu
uliopotea habari njema za ufame wa Mungu na kuwafundisha kuyashika yote
aliyowaamuru na ishara na miujiza itafuatana na waaminio,” alisema
Askofu Kulola.

Kisha akageukia wosia kwa mabinti akisema: “ nakutuma leo ukawaambie
mabinti wacha Mungu, wasimame imara kwa Kristo, najua kuna changamoto
nyingi wanazokutana nazo; lakini bado wanaweza kushinda na zaidi ya
kushinda ikiwa watamtegemea Bwana Yesu, ili siku ya hukumu ikiwa
watakuwepo watakaosema walishinda, basi Yesu aseme mbona hawa waliweza,”
alisema Askofu Kulola.
Mtumishi huyo ambaye alieleza kwamba yeye hakufanya mambo waliyokuwa
wakifanya wenzake enzi zake, aliongeza kwamba, Mungu anaweza kuwatumia
ikiwa watasimama na kuwa na msimamo hata ikiwa ni kwa gharama ya kifo.
Alisema vijana wengi wako makanisani, lakini ni kama wanatumiwa na
ibilisi kutaka kuwaumiza mabinti kwa maelezo ya kutaka kuwaoa, lakini
mwisho wa siku huwageuka na kumwendea mwingine kwa gia hiyo hiyo, huku
akichanganua kuwa ni lazima wawe waangalifu kujua yupi anatoka kwa
Bwana na yupi ni tapeli.
“Kweli nawalilia sana mabinti zangu, namuomba Mungu awape neema ya
kushinda majaribu na vishawishi wa watu wenye nia mbaya, nikienda
Israeli lazima nitafanya maombi kwaajili yao,” alibainisha mtumishi huyo
kwa uchungu.
Mbali na hilo, Askofu Kulola alieleza kwamba anachukizwa na watu
wanaojiita Manabii na Mitume ambao ukiangalia kwa undani utabaini kuwa
wako kinyume na Mungu, ingawa machoni pa wanadamu wanaonekana ni watu
wenye mapenzi mema.
“Kumekuwepo na wimbi kubwa la watu wanaoibuka na kujiita manabii na
mitume, wamekuwa wakielezea watu namna wanavyoweza kuwasaidia kutoka
katika matatizo yao kana kwamba ni waganga wa kienyeji,” alisema
mtumishi huyo na kuongeza:
“Kipindi hiki kama watu hawatokuwa makini ni wazi kuwa watatapeliwa,
kila kitu walicho nacho kwa kudhani kuwa wanamtolea Mungu. Ni vema ikiwa
wachungaji watawafundisha waumini wao Neno la Mungu kwa ufasaha ili
waweze kutofautisha mtumishi wa kweli na tapeli ‘kanjanja.’
Kama
hilo halitoshi mtumishi huyo ambaye yuko kwenye huduma kwa zaidi ya
miaka 50 alisema huu ni wakati wa kila mtu kusimama kwa miguu yake
mwenyewe, badala ya kutegemea mtu mwingine. Huku akichanganua kwamba
Kanisa la Mungu ni lazima liombe kwa bidii ili Mungu alinusuru taifa na
majanga mbalimbali ambayo yanaonekana kutaka kubisha hodi hasahasa kwa
Nchi ya Tanzania,alisema mtumishi huyo.
Toa Maoni Hapa Chini