Mambo ya kuzingatia katika kipindi cha Uchumba.
Na Apostle Darmacy
Baada ya kuwa tumepata maombi ya vijana wengi kutaka
kujifunza habari za Uchumba, nimeona ni vema nikaandaa somo hili ambalo tunaamini litafanyika msaada kwa vijana wengi
ambao wapo kwenye uchumba au wanajiaandaa kuingia katika eneo hili.
Hata hivyo somo hili ni pana sana, kwa sasa nimeandika vitu vichache vya
msingi,
Katika kitabu cha Muhubiri 3:1 Biblia inasema “Kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu”.
Hivyo mwanadamu katika maisha yake hapa chini ya jua kuna vipindi
mbalimbali anavyovipitia hii ni pamoja na kipindi cha uchumba kwa sehemu
kubwa ya watu.
Katika kipindi hiki yapo mambo mengi ambayo wachumba hufanya, mengine
ni mazuri na mengine hayafai kabisa. Na hii yote inatokana hasa na
mitazamo au tafsiri ya uchumba kwa watu husika. Fahamu kwamba tafsiri
unayokuwa nayo juu ya mchumba wako ndiyo inayokuongoza kujenga mahusiano
ya aina fulani pamoja naye.
Lengo la somo hili ni;

Kuongeza ufahamu wa wachumba kuhusu kipindi hiki na Kuwapa vijana
maarifa ya kuwasaidia kuishi kwa nidhamu ya Ki-Mungu katika uchumba wao.
Pia ni kuwafikirisha vijana wanaotarajia kupita katika kipindi hiki
mambo ya kuzingatia. Si wachumba wengi wanajua, Mungu anawataka wafanye
nini katika uchumba wao au kwa lugha nyingine si wachumba wote wanaojua
kwa nini kipindi cha uchumba kipo. Naam katika somo hili nimeandika
mambo hayo kinaga ubaga.
Kwa kuwa suala la uchumba ni pana na lina mitazamo mingi, yafuatayo ni mambo tuliyozingatia katika uandishi wa somo hili;
Kuna makundi mbalimbali ambayo yana taratibu zao kuhusu mchakato wa
mtu kumpata mke au mume kikiwepo kipindi cha uchumba. Makundi hayo ni
pamoja na makanisa, makabila, familia nk.
Wachumba wanaweza kutofautiana kwa kiwango cha elimu, uchumi,
ufahamu juu ya mambo mbalimbali, kikabila, umri na hata kwa rangi pia.
Kuna baadhi ya wachumba hadi kufikia muda wanakubaliana kwamba
watakuja kuishi pamoja walishafahamiana tangu zamani na wengine
hawakufahamiana.
Wachumba wanaweza wakatoka katika madhehebu/makanisa tofauti na hili ni kwa kuzingatia madhehebu/makanisa mengi yaliyopo.
Lengo letu ni kuandika juu ya mwongozo wa Neno la Mungu
katika kipindi cha uchumba. kwa lugha nyingine, je Mungu anataka
wachumba wafanye nini katika kipindi chao cha uchumba?.
Kumbuka uchumba ni kipindi/wakati. Basi kama ni wakati jua kabisa kuna
baadhi ya mambo ambayo ni lazima yafanyike, kwani Biblia inasema katika
Mhubiri 8:5b “ Na moyo wa mwenye hekima hujua wakati na hukumu”, neno hukumu linamaanisha maamuzi, mambo ya kufanya.
Yafuatayo ni mambo ya msingi kufanya katika kipindi cha uchumba;
Jambo la kwanza – Mruhusu Roho Mtakatifu afanyike Bwana wa uchumba wenu
2Wakorinto 3:17 ‘Basi Bwana’ ndiye Roho; na alipo Roho wa Bwana, hapo ndipo penye uhuru’.
Kumbuka Roho Mtakatifu ni msaidizi. Hivyo basi ni vema kumtumia vema
hasa katika nyanja hii ya mahusiano katika kipindi hiki cha uchumba. Ni
Roho Mtakatifu pekee mwenye uwezo wa kukujulisha mambo na siri nyingi
kuhusu mchumba wako hata kama yeye hataki kukueleza. Ukimruhusu Roho
Mtakatifu afanyike Bwana, yeye atakuongoza katIka kufanya maombi
yanayolenga maeneo ya msingi juu ya huyo mwenzako. Kila mtu ameumbwa
pamoja na mapungufu fulani au kwa lugha nyingine mapungufu/ udhaifu
(weakness) ni sehemu ya maisha ya mwanadamu. Roho Mtakatifu anapokuwa
Bwana wa mahusiano yako yeye atakusaidia kuona madhaifu au mapungufu ya
mwenzako kama kitu cha wewe kujivunia(Strength) kwa maana ya kuona
udhaifu wa mwenzako kama kitu chema na si kibaya.
Kumbuka Paulo katika 2Wakorinto 12:9-10. —‘Basi nitajisifia udhaifu
wangu kwa furaha nyingi, ….kwa hiyo napendezwa na udhaifu——- maana
niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu. Hivyo Roho Mtakatifu atabadilisha
tafsiri ndani yako za vyote unavyoona kwa mwenzako huenda juu ya umbile
lake, umri wake, macho yake, kabila lake viwe vitu vya wewe kujivunia.
Zaidi Roho Mtakatifu pia atakuongoza katika maombi yatakayosidia
kuuondoa ule udhaifu ambao umekuja si katika mapenzi ya Mungu, yaani wa
kishetani.
Jambo la pili – ni wakati wa kuweka msingi imara wa uchumba wenu na kufahamiana zaidi.
Hili jambo ni la muhimu kuzingatia. Ni vema wachumba wakatafsiri na
kuelewa vizuri maana ya uchumba. Wachumba wanapaswa kuwa na mipaka
fulani katika uchumba wao na kuwa makini kwa kujilinda na mazingira ya
kila namna ambayo yanaweza yakapelekea wao kuanguka dhambini. Ni vema
mkajua kwamba ninyi ni wachumba na si wanandoa. Na kama ni wachumba basi
uchumba una mipaka yake na hamruhusiwi kufanya mambo ya wanandoa.
Mipaka hii iwe kwa habari ya kutembeleana,kupeana zawadi, mawasiliano
(ingawa mnapaswa kuwa makini na lugha mnazotumia pia) nk. Lengo la
kutafsiri misingi ya mahusiano yenu ni kujiwekea mipaka na mazingira
yatakayowasaidia kuishi maisha ya nidhamu, ushuhuda na kumletea Mungu
utukufu.
Toa Maoni Hapa Chini