Watu wanne wamejeruhiwa katika tukio moja kati ya manne ya milipuko
ya mabomu yakiwamo mawili yaliyolipuka eneo la makanisa mawili visiwani
hapa.
Katika tukio la kwanza, watu wanne walijeruhiwa baada ya
mmoja wao kuokota mabaki ya silaha katika eneo la kufanyia mazoezi ya
kijeshi huko Unguja Ukuu katika Wilaya ya Kusini Unguja.
Eneo hilo liko karibu na pwani na hutumiwa na wanajeshi kwa ajili ya kufanyia mazoezi.
Shabani
Khamis Ibrahim, mmoja kati ya majeruhi wa tukio la Unguja Ukuu,
aliyelazwa katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja, aliliambia NIPASHE kuwa
bomu hilo lililipuka akiwa kwa fundi akitengeneza pikipiki yake.
“Ghafla nilihisi kitu kimenipiga kiunoni na hapo ndipo nilipojihisi kuwa nimeumia na kukimbizwa hospitali,” alisema Shabani.
Majeruhi hao walifikishwa katika hospitali hiyo na watatu hali zao siyo nzuri ingawa mmoja ameruhusiwa.
Majeruhi hao ni Pandu Haji Pandu, Shabani Khamis Ibrahim, Juma Abdallah na Simai Hussein aliyeruhusiwa.
Matukio mengine ya milipuko ya mabomu yametokea katika makanisa mawili na katika mgahawa wa kitalii wa Mercury uliopo Forodhani.
Akizungumza
na NIPASHE, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Mkadam Khamis
Mkadam, alithibitisha kutokea kwa matukio hayo juzi na jana na kwamba
uchunguzi unaendelea.
 |
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mjini Magharibi,Mkadam Khamis Mkadam. |
“Tumefika eneo la matukio na ni kweli kuwa
milipuko iliyotokea ni ya mabomu, ila bado hatujajua ni aina gani ya
mabomu yaliotumika, hivyo ni mapema mno kusema kwani uchunguzi bado
unaendelea,” alisema Kamanda Mkadam.
Matukio hayo yalitokea
katika eneo la Mkunazini, Forodhani na Kijito Upele ambako hadi jana
jioni hakuna mtu aliyekamatwa kuhusiana na matukio hayo.
Mlipuko mwingine ulitokea karibu na Kanisa la Anglikana eneo la Mnara Mmoja saa 7:00 mchana.
Bomu hilo lilichimba barabara, ukuta wa kanisa hilo na kuvunja vioo vya gari moja lililokuwa limeegeshwa eneo hilo.
Mmiliki
wa gari lililokuwa limeegeshwa, Mohamed Ibrahim Ali, alisema kuwa
aliegesha gari lake eneo hilo na kwenda kuswali, lakini aliporejea na
kukuta watu wakiwa wanashangaa mlipuko wa kwanza, aliingia katika gari
laki na ghafla ulitokea mlipuko uliovunja vioo na kumsababishia
michubuko.
Kamanda Mkadam alithibitisha kutokea kwa mlipuko huo, lakini alisema walichukua vipande vya mlipuko kwa ajili ya uchunguzi.
Vile
vile, Kamanda Mkadam alisema juzi asubuhi ulitokea mlipuko nje ya
Kanisa la Assemblies of God katika eneo la Kijito Upele, Wilaya ya
Magharibi wakati waumini wakiendelea na ibada, lakini haukusababisha
athari zozote.
Kuhusu mlipuko uliotokea katika mgahawa wa Mercury
uliopo Forodhani, Kamanda Mkadam alisema lilitokea saa 6:00 mchana jana
mbele ya mgahawa huo na kuchimba ardhini na kwamba wanaendelea na
uchunguzi.


source
Toa Maoni Hapa Chini