 |
Mojawapo ya mabasi yanayotembea nchi kavu na majini. |
- Kwa Afrika, Tanzania itakuwa nchi ya kwanza kuwa na aina hii ya mradi wa mabasi ya majini.
- Mabasi
hayo yana uwezo wa kutembea nchi kavu na majini, hii ina maana kuwa
yatasaidia kwa mfano kusafiri kutoka Posta kwenda maeneo mengine yoyote
ya jiji ambayo yanafikiwa na bahari.
- Mamlaka ya
Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) inasema mradi huo unaweza
kusaidia kuleta mapinduzi makubwa katika sekta ya usafirishaji nchini. inShare
Serikali, mashirika binafsi na wadau wa usafiri
ndani na nje ya nchi wamekuwa wakifanya jitihada mbalimbali kukabiliana
na msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam.
Msongamano huo ambao unachangiwa kwa kiasi kikubwa
na uduni wa miundombinu ikiwemo barabara, umekuwa ni kero kwa wananchi
na Serikali kwa jumla.
Serikali imewekeza katika Mradi wa Mabasi Yaendayo
Kasi (BRT) na usafiri wa treni ndani ya Jiji la Dar es Salaam kama njia
mojawapo ya kumaliza tatizo la msongamano wa magari na foleni.
Msingi wa tatizo
Chanzo kikubwa cha foleni jijini Dar es Salaam si
wingi wa abiria bali ni wingi wa magari binafsi na njia finyu
zisizokidhi mahitaji ya watu walioko katika jiji hilo.
Njia muhimu ya kupunguza foleni na msongamano wa
magari ni kupunguza wingi wa magari barabarani na kuweza kuzipanua
barabara ili kuwe na uwezekano wa kupita kwa urahisi.
Kutokana na foleni na uduni wa huduma za usafiri
wa umma watu wa kundi la kati, wamekuwa wakikimbilia kununua magari
binafsi kwa ajili ya kwenda nayo kwenye shughuli zao kwa urahisi.
Aidha, katika kuendeleza harakati za kupambana na
tatizo la usafiri, Kampuni ya Transevents Marketing ya Tanzania kwa
kushirikana na Kampuni ya Dutch Amphibious Transport Vehicles (DATV) ya
Uholanzi inaendelea na mchakato wa kuleta usafiri wa mabasi ya abiria
yenye uwezo wa kusafiri nchi kavu na majini.
Mkurugenzi Mtendaji wa Transevents, Peter Nzunda
anasema teknolojia hiyo ya mabasi ya nchi kavu na majini (amphibious)
ina lengo la kupunguza tatizo la foleni kwenye barabara za Dar es Salaam
hususan katikati ya jiji kwa kuwa mabasi hayo huweza kupita nchi kavu
na majini.
Hii ina maana kuwa hata katika maeneo yenye
barabara zisizo nzuri au zenye tope, magari hayo huweza kupita hivyo
kutosababisha foleni kama ambavyo hutokea sasa katika baadhi ya maeneo
hasa mvua zinaponyesha na kuharibu barabara.
Anasema mbali na lengo hilo, mabasi hayo
yatatumika kama vivutio vya utalii kwa kufanya utalii wa baharini ambao
kwa Tanzania haujashika kasi, licha ya sehemu kubwa ya nchi kuzungukwa
na maji.
“Mpango huo wa mabasi ya nchi kavu na majini
unalenga kutoa ushawishi kwa watu wa kundi la kati ambao wanatumia
magari binafsi waegeshe magari yao na kutumia usafiri huu ambao utakuwa
wa hadhi yao na unaokidhi haja kwa ubora wake,” anasema Nzunda
“Lengo ni kujenga maegesho ya magari maeneo mbalimbali kandokando ya
bahari, watu wataegesha magari yao na kupanda mabasi yatakayopita majini
kwenda Posta na baadaye kurejea kwa utaratibu huohuo na kuyachukua
magari yao tena kwenye maegesho walipoacha magari yao”.
 |
ANGALIA PICHA YA ITAKAVYOKUWA MARA BAADA YA KUKAMILIKA KWA MRADI WA MABASI YAENDAYO KASI |
“Tunataka pia watu wanaokwenda kwenye fukwe wasiishie kulala na kucheza
mchangani, bali wawe wanapanda mabasi haya na kutembelea sehemu
mbalimbali zenye vivutio baharini; hiyo itakuwa ni fursa ya watu
kuzunguka baharini wakiwa ndani ya mabasi hayo yatakayokuwa katika
miundo tofauti.
Mabasi
hayo yatatumika kwa shughuli za harusi hasa kwa wanandoa ambao
watapenda kufunga ndoa ndani ya maji.Pia yatatumika kwa safari za
kitalii za wafanyakazi wa kampuni mbalimbali, wanafunzi, wanakwaya,
wanavikundi na klabu za mipira.
Usafiri huu utakuwa ni wa bei ya kati ambayo itaendana na huduma
bora na utalenga kuziba changamoto zote ambazo zinapatikana sasa kwenye
usafiri mwingine wa umma,
“Kuna watu wanapanda magari kwa kulipia Sh1,000
badala ya Sh400 kutoka Posta kwenda Mwenge ili kukwepa adha ya kubanana
kwenye daladala zinazokaa muda mrefu kwenye foleni, kwahiyo unaweza
kuona ni kwa namna gani watu wanahitaji huduma bora za usafiri wa umma.”
Katika mazingira ya kawaida familia nyingi jijini
Dar es Salaam zinatumia magari matatu kwa wakati mmoja yaani baba, mama
na mtoto, jambo linaloongeza masongamano barabarani.
Pia usafiri huo utawafanya watu hao
kuyaacha magari yao nyumbani au kwenye maegesho ya magari yatakayojengwa
na hivyo kupunguza kabisa idadi ya magari barabarani.
Mabasi hayo pia yatapunguza gharama za maisha
zinazotokana na matumizi ya mafuta kwani kama mtu anaweza kutumia lita
20- 50 kwa siku.
Serikali inasemaje
Meneja Mawasiliano wa Mamlaka ya Usafiri wa Nchi
Kavu na Majini (Sumatra), David Mziray anasema teknolojia hiyo ya
usafiri wa mabasi ya nchi kavu na majini imekuwa na msaada mkubwa kwa
nchi nyingi Ulaya, kuja kwake Tanzania itakuwa ni habari njema hususan
wakati huu ambapo jiji linakua kwa kasi.
“Kazi yetu ni kupokea maombi na kuangalia kama
yanakwenda sambamba na sheria na kanuni zetu na kama unavyojua hii ni
aina mpya ya usafiri kwa hiyo lazima kutakuwa na mambo ya msingi ya
kuyajadili na kuyapatia ufumbuzi kabla ya kuanza,” Anasema Mziray
Baadhi ya wananchi wanasema mradi huo unaweza kusaidia sana kuondoa kero ya usafiri Dar es Salaam
source
Blogger http://apostledarmacy.blogspot.com


Toa Maoni Hapa Chini